Friday 4 July 2014

TAMKO LA NCCR MAGEUZI KUHUSU UFISADI WA IPTL KUPITIA AKAUNTI YA TEGETA ESCROW

TAMKO LA NCCR MAGEUZI KUHUSU UFISADI WA IPTL KUPITIA AKAUNTI YA TEGETA ESCROW
UTANGULIZI
Itakumbukwa na watanzania kuwa kwa takribani miezi miwili sasa watanzania wamekuwa wakishuhudia bunge la bajeti ambalo pamoja na mambo mengine, hoja ya ufisadi wa fedha za Umma zilizochotwa kifisadi kwenye akaunti ya Tegeta Escrow ilichukua sehemu kubwa ya mjadala wan chi hii. Kama chama tunachukua nafasi hii kumpongeza Mbunge wetu Mhe David Kafulila kwa ujasiri wake wa kutimiza wajibu wake wa kibunge kwa kiwango cha juu kabisa katika kuhakikisha Bunge  linakuwa na udhibiti wa fedha za serikali ambazo ni mali ya Umma.
Aidha, Chama kinachukua nafasi hii kuwapongeza wabunge wote wanaounda Kambi rasmi ya upinzani hususani wa CHADEMA na CUF pamoja na NCCR MAGEUZI kwa ushirikiano wao mkubwa katika kuhakikisha  wanaisimamia serikali katika mambo yote ya msingi likiwemo hili la ufisadi wa fedha za  akaunti ya Escrow. Wameonesha mfano mzuri ndani ya bunge na tunaomba wadau wote wa maendeleo tuungane katika vita hii kwani ni kwa maslahi ya Taifa letu masikini kabisa. Kwa nukta hii tunaomba viongozi wa dini, Asasi za kiraia(NGO), Wanazuoni  watanzania kwa ujumla tuungane pamoja kutaka uwajibikaji ili kudhibiti mzimu huu wa ufisadi wa IPTL/ESCROW ulioanza tangu awamu ya pili ya uongozi wan chi hii na sasa huenda ukaendelea kulitafuna taifa hadi awamu wa tano.
KWANINI ESCROW AKAUNTI ILIFUNGULIWA
Pamekuwa na upotoshaji wa maksudi kabisa kuhusu sababu za kufunguliwa akaunti hii. Upotoshaji huu umefanywa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali bungeni na watuhumiwa wenzake kwa maana ya Maswi na Muhongo kwa maana ya watuhumiwa ambao tayari wamesikika wakizungumzia suala hili. Watuhumiwa hawa wamesikika wakidai kuwa escrow ilifunguliwa kufuatia mgogoro baina ya wabia wa IPTL kwa maana ya Mechmar mwenye 70% na VIP mwenye 30%. Haya wanayapotosha  ili kuhalalisha hoja yao kuwa fedha hizo sio za serikali
NCCR MAGEUZI inapenda Umma wa Watanzania ufahamu kuwa akaunti hii ilifunguliwa na pande mbili; Tanesco na Serikali kwa upande mmoja na IPTL kwa upande wa pili. Na kwamba Akaunti hii ilifunguliwa kufuatia mgogoro wa malipo ya gharama za umeme ambapo Tanesco ililalamika kuwa inatozwa zaidi. Msingi wa Tanesco kulalamika kutozwa zaidi kulitokana na IPTL kudanganya kuhusu mtaji wa asilimia 30% (equity) ambapo ilidai iliwekeza dola 38millioni kumbe iliwekeza dola 50, sawa na Tsh 50,000/= wakati huo mwaka 1995-1998 ambapo exchange rate ya dola kwa Tsh ilikuwa 1; 1000.
Nikatika msingi huo, Mwaka Februari2014 Mahakama ya Usuluhishi wa migogoro ya kibiashara ICSID ilielekeza gharama ziangaliwe upya tangu TANESCO ilipoanza kununua umeme wa IPTL maka 2002 mpaka 2014 ili kuona ni kwa kiasi gani IPTL ilipata fedha isiyostahiki na kiasi gani ilikuwa stahiki ili kuweka msingi wa mgawo wa fedha za escrow. 
Hivyo  Akaunti ya Escrow ilifungulimwa mwaka 2006 ikiwa ni miaka miwili tangu 2004 ambapo TANESCO ilibaini kasoro hiyo ya udanganyifu uliofanywa na IPTL kwenye equity ya dola 38milioni wakaweka dola 50.
KWANINI FEDHA ZA ESCROW NI MALI YA UMMA
Fedha ya Escrow ni mali ya Umma kwa sababu zifuatazo;
1.Ziliwekwa kusubiri kumalizika mgogoro wa gharama ambazo IPTL ilikuwa anatoza TANESCO kifisadi. Mgogoro huo ambao msingi wake ulitokana na IPTL kudanganya kuhusu mtaji wa dola 38milioni kumbe ilikuwa dola50.Mpaka sasa hakuna mahala mgogoro huo umeamuliwa.
2.Ndio sababu Hukumu ya awali ya ICSID ilielekeza pande mbili zifanye hesababu upya ili kubaini ni kiasi gani IPTL ilizidisha na ni kiasi gani ilikuwa halali kwa kuangalia tangu mwaka 2002.  
3.Ndio sababu fedha hizo zilionekana kwenye vitabu vya shirika la Umma Tanesco
4.Ndio sababu Kamati ya PAC, Spika na Waziri Mkuu wote wamelekeza CAG achunguze akaunti hiyo kwani kisheria CAG hana mamlaka ya kuchunguza fedha za wafanyabiashara bali fedha za Umma. Na CAG anachunguza fedha za Umma kwenye makampuni ambayo umiliki wake sio chini ya asilimia 50
MASWI, MUHONGO, MRAMBA, WEREMA NA IPTL NDIO WALISHINIKIZA UFISADI HUU
May 30, 2014 Waziri wa Nishati na Madini Mhe Muhongo alidanganya Bunge kuwa uamuzi wa Serikali kumlipa IPTL/PAP ulikuwa uamuzi wa hukumu ya Mahakama ya Setemba 2013. Ukweli ni kwamba hukumu hiyo hakuna mahala ilielekeza PAP alipwe fedha hizo. Ukweli ni Kwamba uamuzi wa kifisadi wa kutoa fedha hizo ulifanywa na Wizara ya Nishati na Madini na Tanesco kwa upande mmoja na IPTL kwa upande wa pili na ukapewa Baraka na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Hivyo Tunaomba Umma uelewe hivyo.
NYARAKA ZA PAP KUMILIKI ASILIMIA 70 ZA IPTL NI ZA KUGUSHI
Nyaraka za TRA zinaonesha kwamba SingaSinga ambaye ndiye mliki wa PAP alinunua hisa asilimia za 70 za IPTL kutoka kwa PIPERLINK kwa 480millioni, na kwamba PIPERLINK ilinunua Asilimia hiyo 70 kutoka kwa Merchmar kwa Tsh6millioni wakati kampuni hiyohiyo ilinunua asilimia 30 kutoka kwa VIP alinunua kwa 120billioni. Pia inaonesha kwamba kodi ililipwa disemba 6, 2013 wakati alipewa hela za escrow tangu Novemba 2013. Kwa tafsiri nyingine alilipwa fedha za Escrow kabla ya kuwa mmiliki halali wa IPTL.
Na zaidi Umma unapaswa kuelewa kuwa Kwa mujibu wa sheria ya kodi(Finance Act 2012), hisa zinapouzwa kutoka kampuni moja kwenda nyingine uhamishaji huo unathibitishwa na waziri wa wizara husika baada ya kodi kulipwa. Sasa muulizeni waziri wa Nishati na Madini ni lini uhamishaji huo wa hisa aliupitisha kama waziri? Na zaidi taarifa za TRA zinaonesha kuwa kodi ya mauzo ya hisa hizo asilimia 70 kutoka Mechmar kwenda PIPERLINK na Kutoka PIPERLINK kwenda PAP ilipwa tarehe moja yaani Disemba6, 2013.
Huu ni uthibitisho kuwa documents hizi zote ni za kughushi, na watanzania hawawezi kuchezewa akili kiasi hiki.

MKATABA WA WIZARA YA NISHATI NA IPTL KWENDA BOT NI UFISADI
Mkataba huu ulikuwa kifisadi kwasababu hauna msingi wowote wa kisheria wala kimkataba. Mkataba wa kuzitoa fedha hizi ni wa kifisadi mgogoro uliosababisha fedha hiyo iwekwe hapo haukuwa na haujamalizika. Ndio msingi wa hukumu ya mahakama ya ICSID uliotaka mahesabu kufanywa upya. Ikumbukwe kuwa kwa mujibu wa mkataba wa IPTL, pande mbili zilikubaliana kuwa maamuzi kuhusu mgogoro baina yao utamuliwa na mahakama ya ISCID na sio vinginevyo.
MMILIKI WA PAP ANA REKODI YA UFISADI AFRIKA SIO MWEKEZAJI
Kwa mujibu wa report ya wikleaks, Singasinga anaetajwa kuwa mmiliki wa kampuni ya PAP ametajwa katika orodha ya mafisadi waliohusika katika skendo ya ufisadi wa Goldenberg nchini Kenya jina lake likiwa no8 akishirikiana na mtoto wa Rais mstaafu wa Kenya, Gideon Moi. Huu ndio ufisadi mkubwa kupata kufanyika nchini Kenya, uliohusisha Majaji, Viongozi wakubwa kisiasa, familia ya rais na watendaji wakubwa serikalini. Kama CCM haitachukua hatua kali kuhusu ufisadi huu wa escrow ijiandae kufuata nyayo za chama cha KANU kwani kuna kufanana sana kwa skendo hii na ile ya Goldenberg.
KIFO CHA MGIMWA KICHUNGUZWE
Mhe Mbunge David Kafulila, alisisitiza ndani ya Bunge kuwa kama tungekuwa na Bunge makini hata kifo cha aliyekuwa waziri wa Fedha, Mhe Mgimwa kilipaswa kuchunguzwa. Chama kinapenda kusisitiza kauli hiyo kwakuwa Mzee Mgimwa aliugua na kufariki katika kipindi ambacho kulikuwa na shinikizo kubwa la kutoa fedha za escrow bank kuu. Hivyo Kama Chama tunapenda Umma uelewe kuwa huo ndio msingi wetu wa kutaka uchunguzi wa kifo hicho. Na familia ya Mhe Mgimwa tunaipa pole kutonesha madonda lakini tunafanya haya kwasababu ndugu yao alikuwa public figure, alikuwa kiongozi ndani ya nchi hivyo umma una maslahi na chochote kinachomuhusu mtu huyu.
HATMA YA USALAMA WA MBUNGE KAFULILA
Mhe Spika amegoma kuchukua hatua kuhusu mwongozo uliombwa na mbunge Mhe David Kafulila kuhusu kutishiwa maisha ndani na nje ya Bunge. Kama Chama Tunapenda kurejea na kusisitiza kuwa tuna hofu na uhai wa Mbunge wetu hasa kutokana na mazingira yanayozunguka ajenda hii anayoisimamia ikiwa inagusa vigogo na mafisadi wakubwa. Tunao uzoefu wa mazingira kama haya pale kijana Amina Chifupa alipozungumzia madawa ya kulevya, tunao uzoefu na kilichotokea kwa Dr Mvungi alipokuwa mhimili imara wa serikali tatu ndani ya Tume ya warioba, wote tunafahamu kilichowakuta. Kama chama kwakuwa Bunge la vyombo vya dola havioni umuhimu huo, tunamwachia  Mungu, lakini chochote kikitokea tunafahamu ushiriki wa serikali na vyombo vyake.
SPIKA MAKINDA ANADHALILISHA BUNGE
Kazi ya Bunge ni kusimamia Serikali. Ufisadi wa IPTL ulianza tangu awamu ya pili 1994. Ni aibu kwa Spika kukataa Bunge lisichukue jukumu lake la kuichunguza serikali. Wote mnafahamu CAG alivomsafisha Jailo au PCCB ilivosafisha Richmond. Ni katika Msingi huo, Kama chama tunashauri suala hili linalogusa vigogo wakubwa nchini, lichunguzwe na Bunge lenyewe kupitia Kamati teule au uchunguzwe ufanywe na Kampuni za Kimataifa za ukaguzi kama ilivofanyika kwenye fedha za EPA.
Mhe Mbunge alitoa ushahidi wa hukumu ya Septemba 2013 ikionesha dhahili kuwa hakuna mahala hukumu ile ilielekeza IPTL/PAP wapewe fedha hizo za Escrow. Na kuthibitisha kuwa waziri huyu alizungumza uongo bungeni kwa jambo nyeti kama hili, lakini Spika badala ya kutumia kanuni ya kusema uongo anaelekeza mbunge aende PCCB, Kambiwa na nani PCCB wanachunguza uvunjifu wa kanuni za bunge?
Aidha, Ni udhaifu wa Spika huyu ndio sababu haoni aibu kwa Bunge lake kuwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa bodi ya Tanesco. Hii Kamati inawezaje kukosoa uchafu wa TANESCO katika mazingira hayo? Au ndio sababu taarifa ya Kamati hiyo haikuzungumza chochote kuhusu ufisadi wa escrow unaohusu TANESCO na wizara yake?
JAJI WEREMA AJIPIME KAMA ANASTAHILI KUENDELEA KUWA JAJI NA MWANASHERIA MKUU
Uamuzi wa Jaji Werema kutaka kupigana bungeni hata kuzuiwa na Mhe Sitta na Wasira na baadae nje ya Bunge kumtishia uhai Mhe Mbunge ni kielelezo kuwa amepungukiwa sifa za msingi kuweza kuendelea kuwa mwanasheria mkuu wa serikali. Ni aibu serikali ya Kikwete kuwa na Mwanasheria mkuu ambaye kazi yake kubwa ni kuelekeza na kushauri utawala wa sheria nchini harafu anageuka na kuwa mfano wa raia mwenye mapenzi ya kujichukulia sheria mkononi ndani ya bunge na kuahidi kukata kichwa mbunge anaemkosoa. Hii haijapata kutokea katika historia ya Tanzania.
MWISHO
Tunapenda kuhitimisha kwamba tunaitaka Serikali kuchukua hatua madhubuti kuhusu ufisadi huu, na kwamba haturidhishwi na hatua zinazochukuliwa, na kwamba tutafanya utaratibu wa kuwasiliana na vyama ndani ya UKAWA kuona namna bora zaidi ya kulisukuma suala hili ili watanzania waelewe namna nchi yao inavotafunwa. Tunaomba vyama vyote ndani na nje ya UKAWA vitambue ukweli huu kama ambavyo wameanza kutambua ili tusaidiane kuelimisha Umma kuhusu ufisadi huu na watanzania wafanye maamuzi ya nchi yao kwani wanayo haki ya kuhoji na kufaidi utajiri wa taifa lao kwani hawapo kwenye ardhi hii kama wakimbizi au tumbili kama inavyotambuliwa na Serikali ya CCM sasa. Wiki ijayo tutaanza ziara ziara Mkoani Kigoma wakati taratibu zingine zinaendelea kushughulikiwa. Wiki ijayo tutaanza ziara ziara Mkoani Kigoma wakati taratibu zingine zinaendelea kushughulikiwa.
Imesainiwa na;





…………………………….
NYAMBABE
KATIBU MKUU
Julai 03.2014

Monday 24 February 2014

WANACHAMA WA TLP WAJISALIMISHA NCCR-MAGEUZI




Ndugu G. Pwila akipokea kadi kutoka kwa Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Ndg. Mosena J. Nyambabe
akishuhudiwa na Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Ndg. Mussa K. Mussa, Makao Makuu ya Chama Jijini Dar Es Salaam. Tarehe 17 Februari, 2014. Wengine waliochukua kadi ni Ndg. Wallace na Jani. Picha ya chini, wakati wakiondoka.


Sunday 23 February 2014

NCCR-MAGEUZI YAWAKOMBO WANACHAMA WA TLP

Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi Ndg. Mosena J. Nyambabe, akimkabidhi  Kadi ya uanachama Ndugu Wallace, aliyejiondoa katika Chama cha TLP. Katikati ni Naibu Katibu Mkuu (ZNZ), tarehe 17/02/2014 Makao Makuu ya Chama.

Picha ya pili ni Mama Pwila, naye alikuwa miongoni mwanachama walioyepewa kadi siku hiyo.







Saturday 7 September 2013

NCCR YATOA MAONI KUHUSU RASIMU YA KATIBA MPYA

Kaimu Katibu Mkuu wa Chama, Ndg. Mosena Nyambabe akiongea na waaandishi wa habari kuhusu maoni ya chama juu ya Rasimu ya Katiba Mpya ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Friday 30 August 2013

MAONI YA NCCR-MAGEUZI KUHUSU KATIBA MPYA

NCCR-MAGEUZI WAWASILISHA MAONI YA KATIBA MPYA

Chama cha NCCR-Mageuzi leo tarehe 30/08/2013 kimewasilisha maoni kiliyoyakusanya kupitia kwa wanachama na mashabiki wake  kwa kutumia mikutano mbalimbali chini ya kifungu cha sheria Na. 18(1) na (6) Sura ya 83 ya Mabadiliko ya Katiba.
Kwa mujibu wa vifungu hivyo hapo juu, NCCR-Mageuzi ilikuwa baraza la kukusanya maoni kutoka kwa wanachama wake.
Kabla ya kuwasilisha maoni hayo, Kaimu Katibu Mkuu wa Chama hicho Ndugu Mosena J. Nyambabe, alizungumza naWanahabari, ambapo aliwaeleza wanahabari hao kuwa, Chama  kimefurahishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa kuingiza mapendekezo ya NCCR-Mageuzi katika Rasimu hiyo kwa zaidi ya 80%.
Alionesha ibara mbalimbali zilizowekwa na Tume hiyo katika Rasimu hiyo ambazo zinaendana na mapendekezo ya NCCR-Mageuzi.


Tuesday 27 August 2013

MGOMBEA UENYEKITI WA KITENGO CHA WANAWAKE (NCCR-MAGEUZI) AKABIDHIWA FOMU

Ndg. Mosena Nyambabe, Naibu Katibu Mkuu wa Chama, akimkabidhi Mhe. Agripina Buyogela fomu za kugombea Uenyekiti wa Kitengo cha Wanawake, katika uchanguzi mkuu wa Chama utakaofanyika siku chache zijazo. Anayeshuhudia (katikati) ni Ndg. Sebastian Thomas, Katibu wa Ulinzi na Usalama wa Chama - Taifa.
Tukio hili limefanyika makao makuu ya Chama, jijini Dar es Salaam.

Thursday 8 August 2013

Mtihani wa Darasa la Saba nao Majanga!

Kutoka Gazeti la nipashe

8th August 2013

*        Ni wa majaribio katika wilaya 40

*        Maswali mengine yakosa majibu

*        12 yamtoa jasho Profesa UDSM

 

Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia, akiwaonyesha waandishi wa habari (hawapo pichani), mtihani ya kujipima kwa wanafunzi wa darasa la saba uliofanyika Julai 8 na 9, mwaka huu katika wilaya 40 za Tanzania bara.

Madudu zaidi yamebainika katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, baada ya mtihani wa kujipima wa darasa la saba uliofanyika Julai, mwaka huu katika wilaya 40 za Tanzania Bara kuwa na mapungufu makubwa na ya wazi.

Aidha, maswali 12 kati ya 50 katika mtihani wa Hisabati hayana majibu, 14 ni magumu ambayo mtoto wa darasa la saba hawezi kuyajibu na mengine matano yamekosewa na hata yafanywe kwa kiasi gani hayawezi kuwa na majibu.

Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia, alibainisha madudu hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kuwataka Watanzania kushiriki kupinga anguko la elimu linalotia aibu Taifa.

Mbatia alibainisha kuwa katika mtihani huo uliofanywa Julai 8 na 9, mwaka huu, kwa masomo ya Hisabati, Kiswahili na Kiingereza, jina la Wizara limeandikwa ni Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi huku usahihi hakuna neno Stadi.

Alisema matokeo hayo yamekuja katika kipindi ambacho serikali iko katika dhana ya matokeo makubwa sasa (big result now), katika sekta ya elimu na mtihani huo umetungwa kwa dhana hiyo.

Alisema baada ya kupata mtihani huo, alikusanya baadhi ya walimu wa shule za msingi na sekondari katika moja ya shule jijini Dar es Salaam na kuufanya na zaidi ya nusu walishindwa kupata daraja la tatu yaani C.

“Sikuishia hapo, nilimtafuata msomi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) yaani Profesa na kumpa mtihani wa hesabu aliufanya kwa muda wa saa 2:03, lakini na hakupata daraja la kwanza, alishindwa kujibu baadhi ya maswali na mengine kukosa majibu kabisa,” alisema.

Kwa mujibu wa Mbatia, Profesa huyo alisema swali namba 33 ni gumu ambalo linafanywa na mwanafunzi wa fani ya uhandisi na linahitaji muda mrefu kupata jibu.

“Sikutaka kuridhika na majibu yao, nilijifungia ofisini majira ya asubuhi kwa saa 2:30 na kuufanya mtihani wote nikalinganisha na majibu ya wengine, lakini sikupata alama A…ninachojiuliza hii ndiyo Big Result Now?” alibainisha na kuhoji.

Alisema kwa muundo wa mtihani huo, ni kuwakatisha tamaa wanafunzi na kuwafanya wazidi kulichukia somo la hisabati na kiwango cha taaluma nchini kuendelea kuporomoka.

Katika somo la Kiingereza, kulikuwa na mapungufu makubwa ya kisarufi na majina ikiwamo historia ya Tanzania kwa viongozi wa Taifa kama Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Amani Karume.

Mbatia alisema jina la Mwalimu Nyerere limekosewa na kuandikwa Julias na Rais wa awamu ya Pili likiandikwa Ally Mwinyi badala ya Ali Hassan Mwinyi, huku wakishindwa kueleza kifo cha Karume na kueleza kama kifo cha kufanana na Mwalimu Nyerere. Itakumbukwa kwamba, Mwalimu Nyerere alifariki dunia baada ya kuugua wakati Karume aliuawa.

Aidha, alisema katika mtihani wa Kiswahili, kuna mapungufu mengi hususani ya usahihi wa lugha na kuwafanya Watanzania kujiuliza kama mitihani hiyo ilitungwa na wanataaluma walibobea au ni ubabaishaji.

Alisema suala hilo linakwenda sambamba na makosa yaliyopo kwenye vitabu vinavyotumiwa na wanafunzi wa shule za msingi hadi sekondari ambavyo vimepitishwa na kupewa cheti cha ithibati.

“Tumefika mahali pagumu kielimu yaani ni janga la kitaifa,” alisema Mbatia.

Alisema kitabu cha uraia cha darasa la nne, kuna mahali kimeandikwa ‘Serikali za mitaa zinaongozwa na viongozi wa vitongoji’ huku cha hesabu kikieleza namba nzima ni moja hadi 99 badala ya moja hadi tisa.

“Haya yote wanalishwa watoto wa maskini wa nchi hii, hakuna mtoto wa kigogo anayesoma kwenye shule hizi na hawajafanya mitihani hii,” alisema.

MAPENDEKEZO YA MBATIA

Kuundwa kwa tume ya kudumu ya elimu nchini, itakayoshughulika pamoja na mambo mengine, kuhakikisha ubora wa elimu nchini na kudhibiti mambo yote yanayosababisha kutetereka kwa ubora huo (Education quality assurance and control).

Aliongeza kuwa tume hiyo iwe na mamlaka ya kuhakiki utendaji wa taasisi mbalimbali za elimu ambazo hadi sasa zimeonekana kutotimiza vyema majukumu yake.

“Tume itakapoundwa inaweza vile vile kusaidia kubainisha wazi ni nini falsafa na malengo hasa ya utoaji wa elimu nchini kulingana na wakati tulionao,” alisema.

Januari 31, mwaka huu, Mbunge huyo aliwasilisha hoja binafsi bungeni kuhusu udhaifu uliopo katika sekta ya elimu nchini.

Alianisha sura hizo ni kuporomoka kwa uwajibikaji, kutokuthamini rasilimali za Taifa, kukithiri kwa ukiukwaji wa haki za binadamu, kumomonyoka kwa uadilifu miongoni mwa watumishi wa umma na kupungua kwa uzalendo.

Hata hivyo, hoja hiyo haikutiliwa maanani ingawa siku chache baada ya hoja hiyo, Wizara ilifuta Kamati ya Uthibitishaji ya Vifaa vya Elimu (Emac).

Aidha, Februari 18, mwaka huu, Wizara hiyo ilitangaza matokeo ya kidato cha nne yaliyonyesha zaidi ya watahiniwa 240,000 walipata daraja sifuri ikiwa ni asilimia 66 na baadaye matokeo hayo yalipangwa upya na watahiniwa 210,000 wakapata daraja la sifuri.

Kwa mujibu wa matokeo ya ualimu ngazi ya Astashahada na Shahada yaliyotangazwa na Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Julai, mwaka huu, watahiniwa 2,606 wa Stashahada wanarudia mtihani na 533 wamefeli.

Msemaji wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ntambi Bunyazu, alipotafutwa na NIPASHE, alithibitisha mitihani hiyo kufanyika katika halmashauri 40 nchini na kusema kwamba asingeeleza undani wa makosa yaliyobainika hadi atakapopata ufafanuzi wa kitaalam.

Thursday 1 August 2013

NCCR yaigaragaza tena CCM kortini


Chama cha NCCR-Mageuzi kimeendelea kuigaragaza CCM mahakamani, baada ya Mbunge wa Kasulu Vijijini, Mhe. Agripina Zaituni Buyogela (pichani), kuibuka kidedea kwenye rufaa ya kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, yaliyompa ushindi.
Hiyo ni mara ya pili kwa Buyogela, kuibuka kidedea dhidi ya aliyekuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Daniel Nsanzugwanko, aliyekuwa akigombea kiti hicho kupitia CCM.
Nsanzugwanko, alifungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Tabora akipinga matokeo yaliyompa ushindi Buyogela.
Licha ya mambo mengine, Nsanzugwanko alilalamikia mwenendo mbaya na ukiukaji wa Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, huku akimtuhumu Buyogela kuendesha kampeni chafu, kwa kutoa maneno ya kashfa dhidi yake, kuwa ni mchawi aliyeua watu na mwizi. Alidai kwenye mikutano yake, Buyogela alimtuhumu kuwa aliwaua Wabunge wa zamani wa jimbo hilo, Bernard Machupa na Teddy Magayane.
Hivyo, aliomba mahakama hiyo itengue matokeo yaliyompa ushindi na kuamuru ufanyike uchaguzi mdogo, au imtangaze yeye kuwa mshindi. Hata hivyo, Mei 3, 2012, Mahakama Kuu Kanda ya Tabora katika hukumu yake iliyotolewa na Jaji Haruna Songoro, alitupilia mbali madai ya Nsanzugwanko akisema ameshindwa kuyathibitisha pasipo mashaka yoyote.
Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani; Nathalia Kimaro, Salum Massati na William Mandia, walikubaliana na hoja za mawakili wa utetezi na kuamua kutupilia mbali rufaa hiyo.
Habari hii imeandikwa na James Magai wa gazeti la Mwananchi.

Monday 29 July 2013

NDG. EDO MWAMALALA ATEULIWA KUWA KAMISHINA WA CHAMA MKOANI MBEYA

 
Ndugu Edo Makata Mwamalala (pichani) , ameteuliwa kuwa Kamishna wa chama cha NCCR Mageuzi mkoa wa Mbeya.

Barua ya uteuzi wa Mwamalala ya Julai 15, mwaka huu yenye kumbukumbu namba NCCR-M/MM/UTV/102, inesema kuwa Mwenyekiti wa chama Taifa amemteua kuwa Kamishna wa chama katika mkoa huo.

"Napenda kukutaarifu kuwa, kwa mamlaka na madaraka aliyopewa kwa mujibu wa ibara ya 26(2)(f) na ibara ya 37(7) ya Katiba ya NCCR-Mageuzi, toleo la sita sita kama lilivyohaririwa mwaka 2003, Mwenyekiti wa chama Taifa amekuteua kuwa Kamishna wa chama cha NCCR-Mageuzi mkoa wa Mbeya’’ inasomeka sehemu ya barua hiyo.

Barua hiyo iliyosainiwa na kaimu katibu mkuu Ndg. Mosena J. Nyambabe, na kupelekwa nakala kwa Mkuu wa mkoa wa Mbeya, Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya na Wenyeviti wa chama, Majimbo yote ya mkoa wa Mbeya.

Edo Mwamalala, amekiri kupata barua hiyo Julai 25, mwaka huu.

‘’Ni kweli nimepata barua ya uteuzi na ninatarajia kukutana na waandishi wa habari kueleza nia ya chama changu kufanya ziara katika mkoa wa Mbeya’’ alisema Mwamalala.
 
Habari hii imeandikwa na Dordon Kalulunga.
 
Tunampongeza na kumtakia kila la heri katika majukumu yake.

Monday 22 July 2013

NCCR-Mageuzi yaibomoa CCM Kasulu


Mhe. Moses Machali (Mb)
CHAMA cha NCCR-Mageuzi, kimekibomoa Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya kuvuna wanachama wake zaidi ya 200. Tukio hilo lilitokea juzi katika Kijiji cha Nyamidaho, Kata ya Nyamidaho, Jimbo la Kasulu Vijijini, wakati Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR-Mageuzi), alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara kijijini hapo.

Kabla wanachama hao hawajajiunga na chama hicho cha upinzani, Machali aliwaambia kuwa, shida wanazozipata katika maeneo yao, zinasababishwa na CCM ambayo licha ya kuongoza nchi kwa miaka mingi, imeshindwa kutatua kero zinazowakabili wananchi.

Kutokana na hilo, aliwataka wananchi hao wasiendelee kuiunga mkono CCM kwa kuwa kama wataendelea kushirikiana na chama hicho tawala, uwezekano wa maisha yao kuboreka ni mdogo kwa kuwa viongozi wa CCM hawaguswi na matatizo ya wananchi.

“Leo hapa naona kila mmoja anaonekana kuwa na maisha magumu, naona hapa maisha yenu hayatofautiani na maeneo mengine nchini na muelewe kwamba, shida zote hizi zinasababishwa na CCM ambao hawaguswi na shida zenu.

“Kwa maana hiyo, ili muonyeshe kwamba mnaguswa na hampendelei kuwa na maisha magumu, hameni CCM na mjiunge NCCR-Mageuzi kwa sababu hiki ndicho chama kinachoonyesha mwelekeo wa kuwakomboa Watanzania tofauti na vyama vingine vya siasa,” alisema Machali.

Baada ya maneno hayo na mengine, baadhi ya mamia ya wananchi waliokuwa wamehudhuria mkutano huo, walijitokeza kupokea kadi za NCCR-Mageuzi, wakiongozwa na Diwani wa zamani wa Kata ya Nyamidaho kupitia CCM, Mageleyanya Baliyanga.

Wakati huo huo, Machali alisema atawasiliana na Mbunge wa Kasulu Vijijini, Zaitun Buyogela ambaye hakuwa eneo la mkutano, achangie fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kituo cha afya kilichoko katika Kijiji cha Nyamidaho.

Kwa mujibu wa Machali, ujenzi wa kituo hicho ni muhimu kwa afya za wananchi wa kijiji hicho na maeneo ya jirani na kwamba ili umuhimu huo uonekane, kuna kila sababu Buyogela kuchangia ujenzi wa kituo hicho.

Pamoja na hayo, aliwataka wananchi wa Nyamidaho, wasikate tamaa pindi maendeleo yanapochelewa katika maeneo yao, kwa kuwa yanakwamishwa na CCM ambao ni wengi katika vyombo vya maamuzi kama mabaraza ya madiwani na bungeni.